Shirika la Uturuki lapeleka msaada wa chakula kwa familia 8,250 zinazokumbwa na ukame Somalia
Somalia inakabiliwa na uhaba mkubwa wa chakula, huku watu milioni 6.5 wakikadiriwa kuathirika na janga la njaa.
Shirika la misaada ya kibinadamu la Uturuki limepeleka msaada wa chakula kwa familia 8,250 katika maeneo ya Somalia yanayokabiliwa na ukame katika mwezi mtukufu wa Waislamu wa Ramadhan, maafisa wa Uturuki wamesema.
Shirika la Türkiye Diyanet Foundation (TDV) limesambaza vyakula katika majimbo saba na mikoa 13 ya nchi hiyo kama sehemu ya mpango wake wa msaada wa Ramadhan, unaoungwa mkono kupitia michango ya misaada.
Misaada hiyo iliandaliwa kwa familia zinazokabiliwa na ugumu wa maisha wakati wa kiangazi kikali ambacho kimeongezeka katika miaka ya hivi karibuni.
Misaada imesambazwa na wafanyakazi wa Shirika pamoja na waliojitolea katika majimbo tofauti, ikiwemo katika kambi katika mji mkuu wa Mogadishu.
Msaada umetolewa katika kambi ya Hindere katika wilaya ya Daynile na kambi ya Bilhayr katika eneo la Garapaley, huku wahusika wakikutana na familia baada ya kutoa misaada.
Omer Faruk Arslan, mshauri wa huduma za kidini katika Ubalozi ya Uturuki mjini Mogadishu, amesema kwamba msaada wa kibinadamu bado ni muhimu wakati ambapo athari za ukame zimeongezeka nchini Somalia.
“Kutokana na ukame, kumekuwa na matatizo makubwa ya upatikanaji wa chakula na maji katika kipindi cha miaka miwili iliyopita," amesema Arslan.
“Kwa msaada wa wadhamini wetu, tunatoa chakula kwa wale wenye shida katika majimbo 13."
Amesema kila familia itapata kifurushi kimoja na kuongeza kuwa uwasilishaji wa vifurushi 8,250 unatarajiwa kunufaisha takriban watu 80,000, kutegemea na ukubwa wa familia.
Uungwaji mkono wa EU kwa Somalia
Siku ya Alhamisi, Umoja wa Ulaya ulitangaza msaada wa dola milioni 74 za misaada ya kibinadamu kusaidia jamii ambazo ziko katika hali mbaya nchini Somalia huku nchi ikipambana na "hali mbaya ya ukame, migogoro, kukosa makazi na kuongezeka kwa bei ya vyakula."
Katika taarifa, EU imesema fedha hizo zitasaidia katika kuokoa maisha, ikiwemo huduma za afya na lishe bora, matibabu ya utapiamlo, usaidizi wa fedha taslimu, maji, na mpango wa elimu ya dharura.
Tathmini ya kibinadamu inaonesha kuwa takriban watoto milioni 1.85 chini ya umri wa miaka mitano wako hatarini kupata utapiamlo.
EU imesema msaada huo utawasilishwa kupitia washirika wa masuala ya kibinadamu wanaoaminika ambao wapo nchini Somalia ili kuhakikisha msaada huo unawafikia wanaouhitaji kwa wakati.
Tangu 2017, EU imetoa zaidi ya dola milioni 817 kama msaada wa kibinadamu nchini Somalia, taarifa hiyo imesema.