Iran ilisema siku ya Alhamisi kuwa Mlango-Bahari wa Hormuz utaendelea kuwa wazi kwa usafirishaji wa kimataifa lakini “utafungwa” kwa maadui wake na kambi zao katika eneo hilo.
Ali Akbar Velayati, mshauri wa kiongozi mkuu wa Iran Mojtaba Khamenei, aliandika katika mtandao wa kijamii wa X kuwa matokeo ya vita yataamuliwa na mkakati wa Iran badala ya kile alichokiita “ndoto” za wapinzani wake.
“Mlango-Bahari wa Hormuz uko wazi kwa dunia, lakini utabaki kufungwa kwa maadui wa watu wa Iran na kambi zao katika eneo hilo,” alisema.
Velayati aliongeza kuwa vita vitaisha kwa masharti ya Iran.
“Vita vitaisha kwa mkakati na mamlaka ya Iran, si kwa kuchanganyikiwa na dhana zisizo halisi za washambuliaji,” alisema.
Kauli zake zilikuja saa chache baada ya Rais wa Marekani Donald Trump kusema katika hotuba yake kuhusu mwendo wa vita vya Marekani dhidi ya Iran kuwa Iran imebakia na makombora “kidogo sana” na uwezo wake wa kurusha makombora na ndege zisizo na rubani umepungua “kwa kiasi kikubwa.”
Trump alisema anatarajia vita kuendelea kwa wiki mbili hadi tatu zijazo lakini anaamini mgogoro huo unakaribia “kumalizika.”
Iran imeendelea kudumisha udhibiti wa Mlango-Bahari wa Hormuz, njia muhimu ya baharini kwa usambazaji wa nishati kwa mataifa ya Asia, ikiruhusu meli za mataifa ambayo Iran inaita “nchi rafiki” kupita.
Mvutano katika eneo hilo umeongezeka tangu Israel na Marekani walipoanzisha mashambulizi ya pamoja dhidi ya Iran tarehe 28 Februari, yaliyosababisha vifo vya zaidi ya watu 1,340, akiwemo aliyekuwa kiongozi mkuu wa Iran Ali Khamenei.
Iran imejibu kwa mashambulizi ya ndege zisizo na rubani na makombora yakilenga Israel, Jordan, Iraq na nchi za kambi za kijeshi za Marekani zilizoko katika nchi za Ghuba, na kusababisha vifo, uharibifu wa miundombinu pamoja na kuvuruga masoko ya kimataifa na usafiri wa anga.












