Rais wa Kenya aihakikishia nchi usalama huku mvua kubwa ikitishia mafuriko zaidi

Mvua kubwa iliyonyesha Ijumaa Machi 6, 2026 na kuendelea usiku kucha ilisababisha vifo vya zaidi ya watu 62 huku wengi wao wakitoka mji mkuu wa Nairobi

By
Mvua kubwa nchini Kenya imeleta mafuriko katika sehemu mbalimbali za nchi. / others

Rais wa Kenya William Ruto ametoa hakikisho kwa taifa kwamba serikali bado imejipanga kikamilifu kukabiliana na mvua kubwa inayoendelea kunyesha maeneo mbalimbali ya nchi na kusababisha madhara kwa wananchi.

Mvua kubwa iliyonyesha katika mji mkuu wa Nairobi Jumamosi usiku wa Machi 14, 2026, ilisababisha mafuriko katika maeneo kadhaa ya mji mkuu na kutatiza usafiri na shughuli za uokoaji.

Maafisa wa Jiji walisema takriban watu 11 waliokolewa katika maafa hayo.

Haya yanajiri siku chache baada ya mvua kubwa iliyonyesha Ijumaa 6 Machi 2026 na kuendelea usiku kucha, hivyo kusababisha maafa katika maeneo ya nchi ukiwemo mji mkuu Nairobi.

Kufikia sasa serikali imesema idadi ya waliofariki imefikia 62 huku mji mkuu Nairobi ukiwa na idadi kubwa ya vifo.

"Wiki iliyopita, niliagiza kuanzishwa kwa huduma ya pamoja ya mashirika mengi ya dharura, mashirika ya usalama, timu za kibinadamu na idara za kiufundi ili kuratibu juhudi na kudhibiti hali ipasavyo Nairobi na kote nchini," Rais Ruto ameeleza kupitia akaunti zake za mitandao ya kijamii Machi 15, 2026.

"Mashirika husika pia yanasaidia kikamilifu katika shughuli za uokoaji, pamoja na kusafisha mifumo ya mifereji ya maji taka iliyoziba na kurejesha njia za ufikiaji katika maeneo yaliyoathirika," Rais aliongeza.

Kulingana na Wizara ya Mambo ya Ndani nchini humo, utafiti umetambua vitongoji 37 jijini Nairobi vilivyo kando ya barabara kuu za mito na maeneo ambayo yako hatarini kukumbwa na mafuriko.

"Wakati watumishi wa mashirika ya kukabiliana na maafa wakiendelea kuratibu juhudi za kutoa msaada na kukabiliana na maafa, wakazi wanaoishi karibu na bonde na maeneo ya tambarare wanahimizwa kuendelea kuwa waangalifu na kutanguliza usalama wao wakati wa mvua kubwa," Wizara imesema kwenye ripoti yake ya hivi punde kupitia mtandao wa X.

Rais Ruto anasema serikali kuu inashirikiana kwa karibu na serikali za kaunti ili kuhakikisha usalama na ulinzi wa raia wote.

"Serikali itaendelea kuchukua kila hatua inayohitajika kulinda maisha, kusaidia jamii zilizoathirika, na kuhakikisha kuwa hakuna Mkenya anayekabiliwa na changamoto hii peke yake," Rais Ruto alisema.

Aliongeza kuwa chakula cha dharura na msaada wa matibabu tayari vinawasilishwa kwa watu wote walioathiriwa na mafuriko huku serikali ikiendelea kufuatilia kwa karibu hali hiyo.