Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran, Abbas Araghchi, amesema kuwa hakuna mazungumzo yoyote yanayoendelea kati ya Iran na Marekani, akisisitiza kuwa mawasiliano kupitia wapatanishi hakuashirii kuwepo kwa mazungumzo rasmi.
Araghchi amesema viongozi wa ngazi ya juu wa Iran wanaendelea kupitia mapendekezo yaliyowasilishwa, lakini akabainisha wazi kuwa nchi hiyo haina nia ya kuanzisha mazungumzo na Marekani kwa sasa.
Aidha, ameeleza kuwa Iran haitafuti vita, bali inalenga kufikia mwisho wa kudumu wa mzozo uliopo pamoja na kupata fidia kwa uharibifu uliosababishwa.
Kwa mujibu wa Araghchi, Iran tayari imeuonyesha ulimwengu kuwa hakuna nchi inayoweza kutishia usalama wake.
Hapo awali, Iran ilikataa pendekezo la Marekani la kusitisha vita vinavyoendelea, ikisisitiza kwamba azimio lolote litategemea tu masharti na ratiba ya Iran yenyewe.
Iran ilieleza masharti matano muhimu ya kukubali kusitisha mapigano.
Masharti hayo ni pamoja na kusitisha kabisa kile inachoeleza kuwa uchokozi na mauaji, kuanzishwa kwa dhamana ya kuzuia vita kuanza tena, na malipo ya uharibifu na fidia.













