Ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa kulinda amani nchini DRC ulianzishwa mwaka wa 1999. Picha: Getty Images

Shirika la Umoja wa Mataifa la MONUSCO (United Nations Organization Stabilization Mission in the Democratic Republic of the Congo) limeanzisha mchakato wa kuondoa wanajeshi wake nchini DRC.

Mkuu wa MONUSCO, Bintou Keita, alisema Jumatatu katika mkutano na waandishi wa habari huko Kinshasa, mji mkuu wa DRC, kwamba kuondoka kwa ujumbe wa kulinda amani kunafuatia "kufikia hali ya chini kabisa ya mpango wa mpito".

Keita alisema hajui ni muda gani MONUSCO itaondoka DRC, lakini alisema inaweza kutokea kuanzia mwezi Agosti. "Mwishoni mwa Julai, kwa ombi la Katibu Mkuu wa UN [Antonio Guterres], tutawasilisha ripoti ambayo itawezesha kutoa muundo mpya wa ujumbe huko DRC," alisema.

Mkuu wa MONUSCO alisema anatumai "mara tu tutakapoondoka, hatutalazimika kurudi tena".

"Hii ni kwa sababu tunatumai mamlaka ya serikali [katika usalama wa kitaifa] yatarudishwa kikamilifu," alisema Keita.

Aliongeza: "Mchakato wa kuanza kuondoka kwa MONUSCO kutoka DRC tayari umekwishaanza, lakini tunahitaji kuondoka kwa heshima na amani. Hauwezi futa ujumbe kwa siku moja."

Mgogoro wa muda mrefu

DRC imekabiliwa na mgogoro wa muda mrefu, hasa katika sehemu za mashariki ya nchi ambapo makundi ya waasi, ikiwa ni pamoja na waasi wa M23, wamechukua udhibiti.

Mauaji yasiyo halali, ubakaji na uhalifu mwingine wa vita unaonekana katika eneo ambalo halijapata amani kwa muda mrefu.

MONUSCO ilikana madai kutoka kwa baadhi ya watu kwamba ilikuwa inaunga mkono waasi wa M23.

"Tayari tumeshambuliwa na kundi hili. Sielewi kwa nini mnafikiri kwamba tuna mkataba na wao. Hatuko washirika na M23," alisema Keita.

'ADF inapanuka'

Mwakilishi wa UN alisema pia kwamba kundi lingine la waasi, Allied Democratic Forces (ADF), ambalo hivi karibuni lilituhumiwa kwa kushambulia shule ya sekondari magharibi mwa Uganda na kuua zaidi ya watu 37, linapokea ufadhili unaopitia nchi zingine.

Keita alisema ADF inapanuka hadi nchi nyingine, ambapo zoezi la kuajiri linaweza kuendelea.

Serikali ya DRC imekaribisha kuondoka kwa MONUSCO nchini humo, ikisema kuwa kuondoka lazima kuwe "kwa muundo na kwa heshima" ili kuwezesha uhamishaji wa ujuzi kati ya wafanyakazi wanaoondoka wa ujumbe wa kulinda amani na maafisa wa usalama wa ndani.

Patrick Muyaya, Msemaji wa Serikali ya DRC, ambaye pia ni Waziri wa Mawasiliano, alisema hawawezi kuweka muda wa mwisho wa kuondoka kwa MONUSCO nchini humo, kwa sababu kuna "matukio mengi yasiyotarajiwa".

Muyaya aliongea wakati wa mkutano wa pamoja na mkuu wa MONUSCO, Keita.

Kuanzishwa mwaka 1999 MONUSCO ilianzishwa mwezi Julai 1999 baada ya kusainiwa kwa makubaliano ya kusitisha mapigano ya Lusaka kati ya DRC na nchi tano za kikanda - Angola, Namibia, Rwanda, Uganda na Zimbabwe.

Baada ya mauaji ya Rwanda mwaka 1994, baadhi ya wahusika wa vurugu walikimbilia katika eneo la Kivu mashariki mwa DRC. Mwaka 1998, baadhi yao walizindua uasi dhidi ya Rais wa wakati huo wa DRC, Laurent Kabila.

Angola, Chad, Namibia na Zimbabwe waliahidi kumsaidia Kabila kijeshi, lakini waasi waliendelea kuwa na udhibiti wa maeneo ya mashariki.

Rwanda na Uganda inasemekana walikuwa wanaunga mkono harakati ya waasi, Congolese Rally for Democracy (RCD). Ili kuepusha mgogoro hatari wa kikanda, Baraza la Usalama la UN lilitaka kusitishwa kwa mapigano na kuondolewa kwa vikosi vya kigeni. Pia iliwasihi mataifa kutofuatilia masuala ya ndani ya DRC.

Kusitishwa kwa mapigano kulipelekea kuanzishwa kwa MONUSCO.

TRT Afrika