Kenya imeratibiwa kupokea helikopta 16 zilizotengenezwa na Marekani ili kuimarisha uwezo wake wa kutoa amani na usalama wa kikanda/ Picha William Ruto

Na Coletta Wanjohi

TRT Afrika, Istanbul, Uturuki

Rais wa Marekani Joe Biden ameahidi kuitambua Kenya kama mshirika mkuu asiye mjumbe wa NATO (MNNA), yaani Major Non-NATO Ally.

Hadhi hii inatolewa na serikali ya Marekani kwa nchi ambazo zina uhusiano wa kimkakati wa kufanya kazi na Jeshi la Marekani licha ya kuwa sio wanachama wa Shirika la Mkataba wa Atlantiki ya Kaskazini (NATO).

NATO ni muungano wa kisiasa na kijeshi wa nchi 32 kutoka Ulaya na Marekani ya Kaskazini ambazo zimejitolea kulindana dhidi ya tishio lolote.

Hizi ni pamoja na Uturuki, Albania, Ubelgiji, Bulgaria, Canada, Croatia, Jamhuri ya Czech Denmark, Estonia, Finland, Ufaransa, Ujerumani, Uguriki, Hungary, Iceland, Italy, Latvia, Lithuania, Luxembourg, Montenegro, Marekani, Netherlands, Macedonia Kaskazini , Norway, Poland, Portugal, Romania, Slovakia, Slovenia, Hispania, Sweden na Uingereza.

Ina maana gani kwa Kenya kupewa hadhi hii?

Ingawa hali hiyo haijumuishi mkataba wa ulinzi wa pande zote kama ilivyo katika wanachama wakuu wa NATO na Marekani, inatoa fursa mbalimbali za kijeshi na kifedha ambazo hazipatikani kwa nchi zisizo za NATO.

Marekani ina kambi ya jeshi pwani ya Kenya/ Picha: AP

Hatua hii inaipa uwezo Kenya kupata mikopo ya nyenzo, vifaa, au vifaa kwa madhumuni ya utafiti wa ushirika, maendeleo, mazoezi au tathmini.

Itaweza kuwa eneo la Hifadhi ya Vita inayomilikiwa na Marekani kuwekwa kwenye eneo lake nje ya vituo vya kijeshi vya Marekani.

Kenya itapewa kipaumbele kununua silaha za urani. Kuna jumla ya nchi 19 ambazo zimepewa nafasi hii na Marekani. Kutoka barani Afrika, Kenya inaungana na Misri na Tunisia.

Lakini kwa nini Marekani imeichagua Kenya?

Marekani inaiangalia Kenya kama eneo muhimu la kuimarisha amani na usalama barani Afrika na hapo kuzuia kuenea kwa vitendo vya uhalifu dhidi ya Marekani.

Kenya imejikita kama mpatanishi katika mizozo nchini Ethiopia, Sudan Kusini na Jamhuri ya Kidemokraia ya Congo.

Tangu 2011, jeshi la Kenya limekuwa likipambana na kundi la al-Shabab katika nchi jirani ya Somalia.

Kenya itapokea helikopta 16 zilizitengenezwa Marekani / picha AP 

Kambi ya kijeshi ya Marekani iliyoko katika kaunti ya pwani ya Lamu nchini Kenya imekuwa uti wa mgongo wa shughuli za kijeshi za kupambana na waasi.

Marekani imewekeza zaidi ya dola milioni 230 katika ufadhili wa sekta ya usalama na ulinzi wa kiraia tangu 2020, kwa kuzingatia vita dhidi ya ugaidi.

Marekani imeahidi kupanua Uwanja wa Ndege wa Manda Bay katika pwani ya Kenya kwa kujenga barabara ya ndege yenye urefu wa futi 10,000 na hapo kutoa miundombinu inayohitajika ili kuongeza operesheni dhidi ya kundi la kigaidi la al-Shabaab.

Zaidi ya hayo, Kenya iko mbioni kujiunga na Operesheni Gallant Phoenix, mpango ambao unakuza ushirikiano wa kimataifa wa habari dhidi ya ugaidi.

Kenya imeratibiwa kupokea helikopta 16 zilizotengenezwa na Marekani ili kuimarisha uwezo wake wa kutoa amani na usalama wa kikanda. Na kwa mara ya kwanza wanajeshi wa ulinzi wa Kenya wataanza mafunzo katika vyuo vya kijeshi nchini Marekani.

Lakini uhusiano huu kati ya kenya na Marekani una majukumu makubwa. Tayari Kenya imekubali kutuma maafisa wa polisi 1000 nchini Haiti kudumisha amani huku Marekani ikiahidi kuwekeza dola milioni 360 katika ujumbe huu.

Wataalamu wanasema Kenya kutambuliwa kama mshirika mkuu asiye mjumbe wa NATO ni jambo la kifahari lakini pia iwe tayari kwa majukumu yanayoambatana na wadhifa huo.

Bunge la Marekani linatarajiwa kupitisha pendekezo hilo la Rais Joe Biden baada ya siku 30.

TRT Afrika