Joto linapanda leo mjini Algiers katika pambano kali kati robo fainali ya kombe la taifa bingwa Afrika kwa wachezaji wa chini ya miaka 17.
Timu ya Nigeria na Burkina Faso wanapigania nafasi katika nusu fainali ambayo pia itawahakikishia nafasi katika kombe la dunia la wachezaji wasiozidi miaka 17 baadaye mwaka huu.
Wengi wanatazamia Nigeria kuwa na fursa nzuri ya kupenya ila sasa wasiwasi umekuja kwamba Burkina Faso wamefoka katika mechi zao za mchujo na kuonesha ‘na wao wamo!
Ushindi wao dhidi ya mabingwa watetezi Cameroon, uliosababisha kubanduliwa kwao katika mchuoano huu umewaacha wengi vinywa wazi na kuipatia timu hiyo heshima. Wote wawili walimaliza wa pili katika makundi yao.
Kocha mkuu wa Burkina Faso Brahima Traore ana imani na timu yake itafika mbali. ‘‘Lengo letu kuu ni kufuzu kwa kombe la dunia la wachezaji wasiozidi miaka 17. Ninaamini tutaweza’’ amesema Traore.
Rangi nyekundu, njano na Kijani pia zitatawala mitaa ya Algiers wanapo chuana Mali na Jamhuri ya Congo katika mechi ya mwisho ya robo fainali na kuwania nafasi ya mwisho iliyosalia ya kufuzu kombe la dunia la wachezaji wasiozidi miaka 17.
Tayari Morocco na Senegal walisha jinyakulia nafasi katika kombe la dunia litakalo chezwa kuanzia tarehe 10 Novemba – 2 Disemba.
Nigeria wamewahi kushinda kombe la dunia la wachezaji wasiozidi miaka 17 mara tano, 1985, 1993, 2007, 2013 na 2015.
Timu nyingine ya Afrika ambayo ishawahi kushinda kombe hilo ni Ghana, katika miaka ya 1991 na 1995.
Brazil ndio wanaoshikilia ubingwa wa Kombe la dunia la wachezaji wasiozidi 17 ambayo walioshinda 2019. Shindano la 2021 lilifutwa kutokana na janga la Covid 19.