Shirika la Afya WHO linasema Afrika ina upungufu wa wafanyakazi wa afya / Picha: AP

Shirika la Vituo vya Afrika vya Kudhibiti na Kuzuia Magonjwa, Africa CDC, linasema kuwa bara la Afrika lina upungufu wa wafanyakazi wa huduma ya afya ilhali ina asilimia 24 ya changamoto ya maradhi duniani.

"Afrika, Kusini mwa Jangwa la Sahara inabeba asilimia 24 ya mzigo wa magonjwa duniani huku asilimia 3 tu ya wafanyakazi wa afya duniani wakiwa barani Afrika. Hii ni hali ya dharura, lakini ndivyo pia azimio letu," alisema Jean Kaseya, Mkurugenzi Mkuu wa Africa CDC.

Alikuwa akiongea katika mkutano wa "Jukwaa la Uwekezaji la Wafanyakazi wa Afya Afrika" ambalo limeshirikisha mawaziri wa Afrika na wadau zaidi ya 150, kufanya mipango madhubuti ya kuwekeza katika afya ya wafanyakazi.

Mkutano huo uliofanyika Windhoek, Namibia kutoka tarehe 6 hadi 8 Mei, 2024.

Mkutano huo wa kibara umezindua walichoita 'Mkataba wa Uwekezaji wa Nguvu Kazi ya Afya Afrika.'

"Sekta ya wafanyikazi wa afya barani Afrika iko katika njia panda. Uwekezaji mdogo katika mafunzo na kuajiri wahudumu wa afya, pamoja na motisha duni za kuhifadhi nguvu kazi, umesababisha viwango vya bahati mbaya vya uhamiaji, ndani na nje ya bara," alisema Dk Matshidiso Moeti, Mkurugenzi wa WHO Kanda ya Afrika.

Ikiwa na lengo shupavu la kupunguza nusu ya uhaba mkubwa wa wafanyakazi wa afya barani Afrika kwa milioni 5.3 ifikapo mwaka 2030, 'Mkataba wa Uwekezaji wa Nguvu Kazi ya Afya Afrika' utahamasisha na kuunganisha ufadhili wa ndani na ushirikiano ili kuimarisha, kukuza na kuhifadhi nguvu kazi ya afya ya bara hili, haswa katika mazingira ya afya ya vijijini na msingi.

"Kuna haja ya kuwa na mipango iliyoundwa vizuri na kutekelezwa ili kuruhusu wauguzi wasio na ajira kufanya kazi katika maeneo mengine, kusawazisha mtaala ili kuhakikisha kuwa wafanyakazi wa afya kutoka Ghana wanaweza kufanya kazi katika maeneo mengine," Dk. Bernard Okoe-Boye, Waziri wa Afya kutoka Ghana aliwaambia wajumbe wa mkutano.

Wataalamu wanashauri kuwa ni muhimu kwa kila nchi barani kuwekeza zaidi katika mifumo ya afya ya jamii na kusambaza wafanyakazi wa afya ya jamii wanaolipwa, waliofunzwa, walio na vifaa, na wanaosimamiwa ili kusimamia vituo vya afya na kufikia kila familia,

TRT Afrika