| Swahili
AFRIKA
2 dk kusoma
Mpaka wa Burundi na DRC wafunguliwa tena baada ya kufungwa kwa miezi miwili
Mpaka wa Kavimvira–Gatumba ni eneo la kimkakati linalounganisha Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo na mji mkuu wa kibiashara wa Burundi, Bujumbura.
Mpaka wa Burundi na DRC wafunguliwa tena baada ya kufungwa kwa miezi miwili
Burundi ilifungua mpaka wake na DR Congo saa 8:00 asubuhi siku ya Jumatatu baada ya kufungwa kwa miezi miwili. / / Reuters
23 Februari 2026

Burundi imefungua tena mpaka wake wa nchi kavu na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) siku ya Jumatatu, baada ya kufungwa kwa zaidi ya miezi miwili kutokana na mapigano yanayoendelea mashariki mwa Congo.

Mpaka wa Kavimvira–Gatumba, ulioko kwenye mwambao wa kaskazini wa Ziwa Tanganyika, ni njia muhimu inayounganisha Congo na mji mkuu wa kibiashara wa Burundi, Bujumbura.

Mpaka huo ulifunguliwa tena saa 2:00 asubuhi kwa saa za eneo hilo (0600 GMT), kwa mujibu wa gavana wa jimbo la South Kivu, Jean-Jacques Purusi Sadiki, aliyewaambia waandishi wa habari.

Video zilizosambazwa kwenye mitandao ya kijamii zilionyesha wasafiri, wakiwemo wafanyabiashara, wakipanga foleni katika ofisi za uhamiaji tangu alfajiri wakisubiri kuhudumiwa.

Mpaka huo ulifungwa mapema mwezi Disemba baada ya muungano wa waasi wa Alliance Fleuve Congo (AFC/M23), unaojumuisha kundi la M23, kuteka mji wa Uvira mashariki mwa Congo.

Waasi hao walijiondoa mjini humo mwezi Januari kufuatia shinikizo la kimataifa.

Asasi ya Kiraia ya ‘New Congolese Civil Society South-South Kivu’ ilikaribisha kufunguliwa tena kwa mpaka huo na kuwataka wakimbizi wa Congo waliokimbilia Burundi kutokana na kuongezeka kwa mapigano kurejea nyumbani.

Ripoti za mapigano mapya

Kufunguliwa kwa mpaka huo kumekuja wakati kukiwa na taarifa za mapigano mapya kati ya waasi na vikosi vya serikali katika maeneo kadhaa ya wilaya ya Masisi, jimbo la North Kivu.

Kwa mujibu wa asasi za kiraia, mapigano hayo yamesababisha maelfu ya watu kukimbia makazi yao.

Mapema mwezi huu, Rais wa Angola, João Lourenço, alipendekeza usitishaji mapigano kati ya pande zinazozozana mashariki mwa Congo kuanzia tarehe 18 Februari.

Serikali ya Congo ilisema imekubali pendekezo hilo “kwa moyo wa uwajibikaji, utulivu na kutafuta suluhisho la amani kwa mzozo huo.”

Hata hivyo, Ijumaa iliyopita, jeshi la Congo liliwashutumu waasi wa AFC/M23 pamoja na wanajeshi wa Rwanda kwa kushambulia ngome zake katika majimbo ya North Kivu na South Kivu, kinyume na makubaliano ya usitishaji mapigano yaliyopendekezwa na Angola.

Kwa upande wake, msemaji wa waasi hao, Lawrence Kanyuka, siku ya Jumatatu aliishutumu “miungano ya vikosi vya utawala wa Kinshasa kwa kufanya mfululizo wa mashambulizi ya kiholela katika maeneo yenye wakazi wengi ya Rumbishi.”

Kundi la M23 limekuwa kiini cha mzozo mashariki mwa Congo. Kundi hilo linadhibiti maeneo makubwa ya mashariki mwa Congo, ikiwemo miji mikuu ya majimbo ya Goma na Bukavu, iliyotekwa mapema mwaka 2025.

Mji wa Uvira ulihudumu kama mji mkuu wa muda wa jimbo la South Kivu baada ya Bukavu kutwaliwa na waasi.

 

CHANZO:TRT Afrika