Uchaguzi wafanyika Togo baada ya mageuzi ya katiba. / Picha: AP

Raia wa Togo wapiga kura katika uchaguzi wa wabunge siku ya Jumatatu, baada ya mageuzi ya katiba yenye mgawanyiko, ambayo wapinzani wanasema yanamruhusu Rais Faure Gnassingbe kuongeza muda wa utawala wa miongo kadhaa aliyourithi kutoka kwa familia yake.

Uchaguzi huo unakuja baada ya wabunge kuidhinisha mageuzi mwezi huu, ambayo yataunda wadhifa mpya wa uwaziri mkuu, huku wapinzani wanahofia kuwa unalenga kumuongezea Gnassingbe muhula wa kusalia madarakani.

Akiwa madarakani kwa takriban miaka 20, Gnassingbe alimrithi baba yake Gnassingbe Eyadema, ambaye alitawala kwa takriban miongo minne kufuatia mapinduzi yaliyotokea nchini Togo.

Kura ya Jumatatu ni ya kuwachagua wabunge 113 na pia kwa mara ya kwanza manaibu 179 wa mikoa kutoka wilaya tano za nchi, ambao pamoja na madiwani wa manispaa watachagua baraza la mawaziri lililoundwa hivi karibuni.

Wabunge kuchagua rais

Kwa chama tawala cha UNIR mfumo huu utaifanya Togo kuwa na uwakilishi zaidi, lakini vyama vya upinzani vimewahamasisha wafuasi kupiga kura dhidi ya kile wanachosema ni "mapinduzi ya taasisi."

"Tunataka kujitokeza kwa wingi siku ya Jumatatu ili tuweze kutoa nafasi kwa upinzani kushinda na kuchukua udhibiti wa bunge," alisema Afi Akladji, muuza viatu na mfuasi wa chama kikuu cha upinzani cha ANC.

Gnassingbe, 57, tayari ameshinda uchaguzi mara nne, ambao mara zot ulipingwa na upinzani na kutajwa kuwa na dosari. Aidha angeweza kuwania tena urais mwaka wa 2025 kulingana na katiba ya hapo awali.

Kulingana na katiba mpya iliyopitishwa na wabunge mnamo Aprili 19, rais wa Togo amechaguliwa na bunge na sio wananchi, kama rais na cheo ambacho hakina mamlaka, kwa muhula wa miaka minne.

Kuboreshwa kwa miundombinu

Togo inahama kutoka mfumo wa urais hadi mfumo wa bunge, hii ikimaanisha kuwa mamlaka inashikiliwa na rais mpya wa baraza la mawaziri, ambaye moja kwa moja atakuwa kiongozi wa chama kilicho wengi katika bunge jipya.

Chama tawala cha UNIR, tayari kinatawala bunge. Ikiwa kitashinda uchaguzi Jumatatu, Gnassingbe anaweza kuchukua wadhifa huo mpya.

Kwa wafuasi, kurefusha muda wa Gnassingbe kunamaanisha kuendelea na mipango yake ya maendeleo, ambayo wanasema imeboresha miundombinu.

"Tuna barabara, hasa mji mkuu wa Lome, shule zimejengwa, miradi imeanzishwa kwa ajili ya wanawake, vijana na wakulima," alisema Evariste Yalo mwenye umri wa miaka 31, fundi kompyuta na mwanaharakati wa UNIR.

Misheni za waangalizi

"Nchi inaenda, katika njia sahihi. Ndio maana rais lazima aendelee."

Jumuiya ya kanda ya Afrika Magharibi ECOWAS ilisema itatuma timu ya waangalizi nchini Togo kufuatilia upigaji kura.

Majaribio ya upinzani kuandaa maandamano dhidi ya mageuzi hayo yalizuiwa na mamlaka.

Mamlaka ya Juu ya Sauti na Mawasiliano ya Togo (HAAC) pia ilisimamisha kwa muda uidhinishaji wote kwa vyombo vya habari vya kigeni ili kuripoti uchaguzi.

TRT Afrika