Rais wa Misri Abdel Fattah el Sisi alisema anathamini ofa ya Rais wa Marekani Donald Trump ya kuingilia kati mzozo kuhusu maji ya Mto Nile kati ya Misri na Ethiopia.
Katika ujumbe kwenye X, Sisi alisema Jumamosi kwamba alijibu barua ya Trump kwa kuthibitisha msimamo wa Misri na wasiwasi kuhusu usalama wa maji ya taifa kuhusiana na Bwawa Kuu la Ethiopia (GERD), ambalo linasababisha mzozo.
Siku ya Ijumaa, Trump alisema yuko tayari kuanzisha upya upatanishi wa Marekani kati ya Misri na Ethiopia ili kutatua mzozo kuhusu bwawa la Ethiopia, ambalo Misri na Sudan zinaona kuwa tishio kubwa kwa usambazaji muhimu wa maji.
Misri imekuwa ikipinga mradi huo kwa muda mrefu kutokana na hofu kuhusu usambazaji wake wa maji ya Nile baadaye, kwa sababu inategemea mto huo kwa kiwango kikubwa. Sudan, nchi nyingine iliyoko chini kwa mto, imeonyesha wasiwasi kuhusu udhibiti na usalama wa usambazaji wake wa maji na mabwawa.
Kiongozi wa jeshi la Sudan, Abdel Fattah al-Burhan, pia alikaribisha ofa ya kuingilia kati ya Trump Jumamosi.
Ethiopia, taifa lenye idadi ya pili kubwa ya watu barani Afrika lenye watu zaidi ya milioni 120, linaona bwawa hilo la dola bilioni 5 kwenye tanzu ya Nile kama sehemu ya mipango yake ya kiuchumi. Limekuwa likikataa madai ya Misri mara kadhaa.














