| Swahili
UTURUKI
4 dk kusoma
Uturuki yapinga vikali hatua yoyote ya kijeshi dhidi ya Iran
Waziri wa Mambo ya Nje wa Uturuki amesema matatizo ya kiuchumi ya Iran yanatokana na vikwazo vilivyowekwa dhidi ya nchi hiyo, na kwamba Iran kutatua matatizo na "baadhi ya wadau" kuntanufaisha pia Uturuki.
Uturuki yapinga vikali hatua yoyote ya kijeshi dhidi ya Iran
Fidan alisema kuwa vikwazo vya kiuchumi husababisha huduma fulani za msingi kupungua au kukosekana. / / AA
15 Januari 2026

Uturuki inapinga kabisa aina yoyote ya uingiliaji wa kijeshi dhidi ya Iran, amesema Waziri wa Mambo ya Nje wa Uturuki, Hakan Fidan.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Istanbul, Fidan alisema Uturuki haitaki kuona nchi yoyote ikiingilia mambo ya ndani ya Iran kijeshi, na akaitaka Iran itatue matatizo yake ya ndani yenyewe.

"Kwa kuangalia kwa karibu, hakuna hali ambayo inaweza kuchochea hamu ya baadhi ya nchi zenye uhasama na Iran kuongeza uadui dhidi ya nchi hiyo. Hata hivyo, matatizo ya kiuchumi yanayotokana na sera zilizopo na kutokuwa na uwezo wa kuzitatua zimesababisha matatizo makubwa. Hatutaki kuona uingiliaji wowote wa nje hapa," Hakan Fidan aliwaambia waandishi wa habari mjini Istanbul.

Akiashiria kauli za hivi karibuni za Rais wa Marekani Donald Trump, Fidan alisema kuwa hadi sasa hakujawa na dalili za wazi za Marekani kutaka kutumia majeshi ya ardhini dhidi ya Iran.

Kuhusu maandamano ya hivi karibuni nchini Iran, Fidan alisema kuwa vikwazo vya kiuchumi husababisha huduma fulani za msingi kupungua au kukosekana. Alieleza kuwa “Iran ina idadi kubwa ya watu na jamii inayobadilika, yenye wananchi waliostaarabika na wenye hamu kubwa ya kushiriki katika maisha ya kijamii. Unapowanyima jamii kama hiyo fursa mbalimbali, matatizo ya aina hii hujitokeza.”

Aliongeza kuwa “Mara nyingi mateso yanayosababishwa na matatizo ya kiuchumi hutafsiriwa kama ni uasi wa kiitikadi dhidi ya utawala, ilhali kwa uhalisia ni suala tata lisilo wazi moja kwa moja.”

Fidan alisisitiza kuwa Iran ni muhimu sana kwa Uturuki, akisema kuwa kila kinachohusu Iran kinaihusu pia Uturuki. Aliongeza kuwa Iran kutatua matatizo yake na wadau fulani wa kimataifa kunainufaisha Ankara.

Akieleza kuwa amewahimiza viongozi wa Iran kutatua matatizo yao na nchi nyingine, Fidan alisema, "Inapaswa kutatua masuala yake kuhusu suala la nyuklia kwa njia ya diplomasia bila kupoteza fursa yoyote ili matatizo fulani ya kimuundo yanayosababisha matatizo ya kiuchumi yaweze kuondolewa."

Uturuki itaendelea kufuatilia yanayojiri na juhudi zake za kidiplomasia na Iran, alisema.

Syria

Kundi la kigaidi la YPG linaendelea kuwa "tishio kwa kanda na kwetu," Fidan alisema, akiongeza kuwa Uturuki haina matatizo na Wakurdi nchini Syria, lakini ina tatizo na kundi la kigaidi ambalo linaendesha shughuli zake katika nchi nne kwa majina tofauti.

"Tunataka makubaliano ya Machi 10 kutekelezwa, hata kama yatakuwa na matatizo," alisema, akimaanisha mapatano ambayo Uturuki na serikali ya Syria wamesema kuwa YPG imekiuka makubaliano hayo.

Fidan alisema Uturuki inashangazwa kuona baadhi ya nchi zinazungumzia uhusiano "uliogunduliwa" kati ya YPG na kundi la kigaidi la PKK, akiongeza kuwa uhusiano wao "umekuwa ukijulikana kwa muda mrefu."

Akitoa mfano wa ghasia za hivi majuzi katika mji wa Aleppo, alisema, "Kuhusu Aleppo, tulionya kwamba mchakato huo haupaswi kufikia kiwango cha kutumiwa kwa silaha. Huu ni mtindo unaorudiwa mara kwa mara. Kuanzia Tel Rifaat na Ayn al-Arab, tuliweka wazi kuwa uwepo wao huko ni kinyume cha sheria. Ikiwa wanataka kuonyesha nia njema, ni lazima waingie katika mchakato unaozingatia diplomasia na kufanya mazungumzo. Aliongeza kuwa kundi hilo halina uwezo wala mtazamo wa kushughulikia wadau wengi katika mazingira magumu kama hayo.”

"Uwakilishi wa walio wachache katika katiba ya Syria ni muhimu. Lakini tatizo kubwa ni pale makundi yanapojaribu kushiriki kama vyombo vya kisiasa vinavyojitenga. Alisema kuwa kuishi chini ya bendera moja huku kila kundi likihifadhi utambulisho wake na kunufaika sawa na rasilimali za taifa ni njia bora zaidi. Kugawanya nchi katika maeneo ya kisiasa kunaweza kusababisha kuporomoka kwa nchi, jambo linalohitaji tahadhari kubwa," Fidan aliongeza.

YPG ni tawi la Syria la kundi la kigaidi la PKK.

Ukraine

Kuhusu vita vya Urusi na Ukraine, Fidan alisema kuwa ikiwa makubaliano ya amani yatafikiwa, majeshi ya majini ya Uturuki yatakuwa na jukumu la kuongoza usimamizi wa usalama katika Bahari Nyeusi.

"Ikiwa makubaliano ya amani yatafikiwa, yatakuwa na vipimo vitatu: jinsi amani itakavyosimamiwa, jinsi uwezo wa kujilinda kwa Ukraine utakavyodumishwa, na ni hatua gani zitachukuliwa iwapo makubaliano yatakiukwa. Kijeshi, amani ina maeneno matatu: ardhi, anga, na bahari. Bahari Nyeusi ni eneo ambalo linahusu Uturuki moja kwa moja," aliongeza.

"Vita vya Urusi na Ukraine na mabadiliko katika mahusiano katika eneo la Atlantiki yamefanya usalama wa Umoja wa Ulaya uzidi kutiliwa shaka. Uturuki, inayoongozwa hasa na Rais wetu Recep Tayyip Erdogan, imeweka juhudi kubwa katika mchakato huu. Juhudi hizi zitaendelea pia katika mwaka 2026," alisema.

CHANZO:AA
Soma zaidi
Rais wa Uturuki awasili Ethiopia kwa ziara rasmi
Emine Erdogan awatuza wasukuma mabadiliko wakati wa makala ya 7 ya tuzo za TRT World
Rais wa Uturuki aelekea Ethiopia kwa ziara ya kikazi
Waziri Mkuu wa Somalia apongeza uchimbaji mafuta wa 'kihistoria' baharini na Uturuki
Uturuki inapanua utaalam wa reli, kutoa mafunzo kwa wafanyakazi Afrika, Asia
Erdogan: Uturuki inaendelea kutafuta amani ya kanda licha hofu iliyopo ulimwenguni
Rais wa Uturuki ateuwa Waziri mpya wa Katiba na Mambo ya Ndani katika mabadiliko ya Baraza la Mawazi
Fidan wa Uturuki akataa mashambulizi ya anga kama njia ya kubadilisha uongozi wa Iran
Makamu wa Rais wa Uturuki akutana na balozi wa Brazil
Idadi ya watu nchini Uturuki yafikia milioni 86 kwa mwaka 2025
Uturuki yalaani shambulizi la RSF nchini Sudan
Matetemeko ya ardhi ya Uturuki 2023 yalisababisha hasara ya dola bilioni 250: Erdogan
Fidan wa Uturuki akutana na Kamishna wa Maswala ya Wanachama wa EU, kujadili masuala ya ushirikiano
Rais wa Uturuki aadhimisha kumbukumbu ya miaka 3 ya tetemeko la ardhi
Uturuki imelaani shambulizi la kigaidi nchini Nigeria lililoua takriban watu 170
Uturuki kuimarisha uwepo wake wa kijeshi kuisaidia Somalia kupambana na ugaidi
Uturuki na Saudi Arabia kuimarisha ushirikiano wa ulinzi na uwekezaji katika ndege za kivita za KAAN
Mke wa Rais wa Uturuki amekutana na mwenzake wa Misri jijini Cairo
Erdogan na Sisi waimarisha ushirikiano kati ya Uturuki na Misri wajadili Gaza na migogoro ya kikanda
Kikao cha mwisho cha Jukwaa la Biashara kati ya Uturuki na Misri chafunguliwa jijini Cairo