Mtanange uliokuwa ukisubiriwa kwa hamu sana na wapenda soka hasa Afrika mashariki kati ya Morocco dhidi ya Tanzania katika hatua ya mtoano 16 bora AFCON 2025, ulimalizika kwa Tanzania kutolewa baada ya ushindi mwembamba wa Morocco wa goli 1-0.
Katika kipindi cha kwanza Morocco walianza mchezo kwa kasi wakishambulia ili kupata bao la kuongoza, lakini safu ya ulinzi ya Tanzania ikiongozwa na Ibrahim Abdallah ilikaa imara na kuzuia mashambulizi.
Tanzania walifanya mashambulizi kadhaa na kufika ndani ya ‘boxi’ la Morocco, lakini hawakuweza kutikisa nyavu.
Dakika 45 za awali zilimalizika mambo yakiwa magumu. Mbali na Morocco kushambulia kwa kasi lakini safu ya ulinzi ya Taifa Stars ilidhibiti mashambulizi hayo ya ‘Simba wa Atlas’
Kipindi cha Pili: Baada ya timu kusomana sasa ni dakika 45 za maamuzi.
Kama ilivyotegemewa na wengi kipindi cha pili hakikuwa rahisi kwani timu zote zilikuja na mbinu ya kujihami, japokuwa walicheza mpira wa kufunguka Morocco walitandaza pasi nyingi wakitegemea wanaweza kuvuka ngome za Tanzania.
Baada ya timu zote kusomana kimchezo, kilichobaki kilikuwa ni kutumia mbinu zaidi ili kuhakikisha ushindi unapatikana. Bado milango ilikuwa migumu maana golikipa nambari 1 wa Tanzania Hussein Masalanga alifanya jitihada za kipekee kulinda lango lake.
Baada ya vuta nikuvute ya bila bao hatimaye mnamo dakika ya 64 ya mchezo bao la kwanza likapatikana kupitia Brahim Diaz na kuifanya Morocco kuchungulia robo fainali ya AFCON 2025.
Dakika 90 za mpambano ziliisha kwa ushindi wa bao 1-0 kwa Morocco, na kuwafanya kusonga hatua ya mbele ya michuano na watakuwa wanasubiria kujua mpinzani wao katika robo fainali kati ya Afrika Kusini au Cameroon.














