Rais wa Uturuki Recep Tayyip Erdogan ametoa wito kwa Uturuki kurejeshwa kwenye mpango unaoongozwa na Marekani wa ndege za kivita za F-35, akisema hatua hiyo itasaidia kuimarisha uhusiano kati ya Uturuki na Marekani, na pia kuimarisha usalama wa NATO.
Katika majibu ya maandishi kwa maswali kutoka Bloomberg, akieleza kuhusu mkutano wake wa Septemba 2025 na Rais wa Marekani Donald Trump katika Ikulu ya White House, Erdogan alieleza uamuzi wa kuiondoa Uturuki katika mpango wa F-35 kutokana na nchi hiyo kununua vifaa vya kijeshi Urusi karibu mwongo mmoja uliopita “siyo haki,” akiongeza kuwa yeye mwenyewe amemfahamisha Trump kuhusu hilo.
Rais wa Uturuki anasema kurudi madarakani kwa Trump kuliweka fursa ya uhusiano kati ya Uturuki na Marekani kufikia “hatua nzuri na yenye tija.”
Kuhusu suala la ndege za F-35, Erdogan amesema: 'Kupokea kwa ndege za F-35 ambazo Uturuki tayari imeshazilipia na kurejeshwa kwenye mpango huo, ni muhimu na wajibu” kwa uhusiano bora wa ulinzi na Marekani na NATO.
Kuhusu uwezekano wa kununua ndege 70 za F-16 kutoka kwa Marekani, Erdogan alisisitiza kuwa Uturuki inategemea kuwa makubaliano yatakuwa na utashi wa muungano wa NATO, akieleza mfano wa Uturuki wa kununua ndege za Eurofighter.
Kuhusu kesi ya jinai nchini Marekani dhidi ya benki ya serikali ya Uturuki Halk Bankasi AS, Erdogan alisisitiza kuwa Uturuki inachukulia madai hayo kutokuwa na msingi na imeanzisha mazungumzo kuhakikisha benki hiyo haikabiliwi na utozwaji faini “usio wa haki.” Alisema: “ Matumaini yetu ni kuwa tutafikia makubaliano mazuri ambayo yako kwa misingi ya sheria.”
Kuhusu uhusiano wa mataifa mawili juu ya suala la nishati, kiongozi huyo wa Uturuki alisema: “Tumeongeza kwa kiasi kikubwa ununuzi wetu wa LNG, hasa kutoka Marekani,” akisisitiza kuwa hilo sasa lina “nafasi muhimu” kwa manunuzi ya Uturuki.
Erdogan ameeleza kuwa msimamo wa Uturuki uko wazi, akisema: “Tunazingatia maslahi ya taifa letu na usalama wetu wa nishati.”
“Kama nchi ambayo inategemea kwa kiasi fulani kuagiza sehemu ya gesi ya haidrokaboni, lazima tuwe makini katika masuala yote ambayo yataathiri usalama wetu wa nishati,” amesema.
Uturuki ‘ndiyo pekee inaweza kuzungumza moja kwa moja’ na Urusi, Ukraine
Alisisitiza kuwa kutokana na Uturuki kutoegemea upande wowote katika vita vya Urusi na Ukraine, imejiweka katika nafasi nzuri ya kuwa mwenyeji wa mazungumzo ya baadaye ya amani na inaweza kusaidia kufuatilia kusitishwa kwa mapigano kati ya mataifa hayo mawili yanayozozana.
“Uturuki ndiyo nchi pekee inayoweza kuzungumza moja kwa moja” na Rais wa Urusi Vladimir Putin na Rais wa Ukraine Volodymyr Zelenskyy, Erdogan alisema: “Milango yetu iko wazi kwa wote. Nimeeleza msimamo huu wazi na mara kadhaa kwa viongozi” wote wawili.
Erdogan pia alishtumu vikali hatua za Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu huko Palestina, akisisitiza kuwa Kikosi cha Kimataifa cha kuleta amani Gaza kilichopendekezwa “kitapata tabu kukubaliwa” bila Uturuki kuwepo.
“Tuko katika nafasi kama nchi muhimu kwenye operesheni kama hiyo kutokana na uhusiano wetu wa kihistoria wa muda mrefu na upande wa Palestina, masuala ya usalama na ya kidiplomasia tuliokuwa na Israel katika siku zilizopita, na ushawishi wetu katika kanda kama nchi mwanachama wa NATO,” alisema.
“Utashi wetu wa kisiasa uko wazi; tuko tayari kuchukuwa jukumu lolote kwa lengo la kupatikana kwa amani ya kudumu Gaza,” alieleza.



























