| Swahili
AFRIKA
2 dk kusoma
Wakenya hawatapigania tena Urusi nchini Ukraine, Mudavadi anasema akiwa Moscow
Ripoti ya kijasusi ya Kenya iliyowasilishwa kwa wabunge mwezi Februari ilisema kuwa zaidi ya Wakenya 1,000 wameajiriwa kupigana upande wa Urusi katika vita vya Ukraine, mara tano zaidi ya mamlaka ilivyokadiria hapo awali.
Wakenya hawatapigania tena Urusi nchini Ukraine, Mudavadi anasema akiwa Moscow
Waziri wa Mambo ya Nje wa Kenya Musalia Mudavadi ameshauriana na mwenzanke wa Urusi Sergei Lavrov / Reuters
tokea masaa 3

Waziri wa Mambo ya Nje wa Kenya Musalia Mudavadi alisema Jumatatu kwamba Moscow na Nairobi zilikubaliana kwamba raia wa Kenya hawatapigania tena Urusi nchini Ukraine.

Mudavadi alitoa kauli hiyo baada ya kufanya mazungumzo na Waziri wa Mambo ya Nje wa Urusi Sergei Lavrov mjini Moscow.

"Mheshimiwa amezungumza nasi kuhusu ustawi wa Wakenya ambao wako nchini Urusi na haswa wale ambao wanahusika katika operesheni hiyo maalum," Mudavadi alisema.

"Na ninataka kueleza wazi kwamba sasa tumekubaliana kwamba Wakenya hawataandikishwa kupitia Wizara ya Ulinzi (ya Urusi) - hawatastahiki tena kuorodheshwa," alisema. "Hakutakuwa na usajili zaidi."

Aliongeza kuwa huduma za kibalozi zitaandaliwa kwa Wakenya wanaohitaji usaidizi kupitia njia zinazofaa za kidiplomasia.

"Hatutaki kwa sababu yoyote ile ushirikiano wetu na Urusi ⁠ufafanuliwe kutoka kwa lensi za ajenda ya operesheni maalum (nchini Ukraine) pekee," alisema. "Uhusiano kati ya Kenya na Urusi ni mpana zaidi kuliko huo."

Lavrov alisema kuwa raia wa Kenya walikuwa wametia saini kwa hiari mikataba ya kupigana pamoja na jeshi la Urusi.

Ripoti ya kijasusi ya Kenya iliyowasilishwa kwa wabunge mwezi Februari ilisema kuwa zaidi ya Wakenya 1,000 wameajiriwa kupigana upande wa Urusi katika vita vya Ukraine, mara tano zaidi ya mamlaka ilivyokadiria hapo awali.

Wanasiasa wa Kenya wameelezea kile wanachosema ni mtandao wa maafisa walaghai wa serikali ambao wameshirikiana na mashirika ya ulanguzi wa binadamu kuwaajiri Wakenya kupigania Urusi nchini Ukraine, tabia ambayo Nairobi ilisema ilitaka kukomesha.

CHANZO:reuters