Ajali hiyo ilitokea majira ya saa nane usiku wakati treni hiyo ilikuwa safarini katika safari ya takriban kilomita 200 kutoka mji wa Dewele, ulioko karibu na mpaka wa Djibouti, kuelekea mji wa Dire Dawa. Maafisa wa eneo hilo walieleza kuwa ajali hiyo ilisababisha maafa makubwa kwa abiria waliokuwa wakisafiri na treni hiyo.
"Ajali iliyotokea katika reli ya Dire Dawa-Dewele imewaua watu 14 na kujeruhi wengine 29, baadhi yao wakiwa na majeraha makubwa," ilieleza taarifa ya Dire TV iliyochapishwa kwenye ukurasa wao wa Facebook, bila kutoa maelezo ya kina kuhusu chanzo cha ajali hiyo.
Picha zilizosambazwa na chombo hicho cha habari zilionyesha mabehewa ya treni yakiwa yamepinduka, mengine yakiwa yamesvunjika, jambo linaloashiria ukubwa wa tukio hilo.
Ajali za treni si za kawaida nchini Ethiopia
Ajali za treni si jambo la kawaida nchini Ethiopia, taifa lenye idadi ya watu takriban milioni 130, na ambalo linashikilia nafasi ya pili kwa idadi ya watu barani Afrika.
Ajali kubwa ya mwisho ya treni nchini humo iliripotiwa mwaka 1985, ambapo zaidi ya watu 400 walipoteza maisha na wengine 500 kujeruhiwa baada ya treni iliyokuwa ikitokea Djibouti kuelekea Addis Ababa kuanguka kwenye korongo.