Rais wa Uturuki, Recep Tayyip Erdogan, alisema kuwa Uturuki imeazimia kubaki mbali na mzozo hatari unaoendelea unaohusisha Israel na Iran, akionya kuwa mzozo huo unaweza kugeuka kuwa vita vya muda mrefu vya uhasama katika eneo lote.
Akizungumza baada ya mkutano wa baraza la mawaziri jijini Ankara, Uturuki, Erdogan alisema kuwa Uturuki inasimamia hali hiyo kwa uangalifu kupitia mbinu aliyoielezea kama ya tahadhari na busara, ikiongozwa na “hekima ya taifa”.
“Tumeazimia kuweka nchi yetu mbali na mzozo hatari unaoendelea,” alisema Erdogan, akisisitiza kuwa Uturuki haitaki vita hiyo vibadilike na kuwa mzozo mpana zaidi kati ya nchi za eneo hilo.
Aliongeza kuwa Uturuki imejitokeza kama mojawapo ya nchi zilizotathmini kwa usahihi mgogoro unaoendelea na inachukua hatua kwa uwajibikaji katika mazingira tete ya kisiasa na kijiografia.
“Uturuki ni miongoni mwa nchi zinazoshifiwa kwa kusoma kwa usahihi mchakato uliolijaza eneo letu harufu ya damu na baruti,” alisema.
Erdogan pia alisisitiza kuwa Uturuki haitaingia kwenye kile alichokiita mitego inayolenga kuvuta nchi hiyo ndani ya mzozo.
“Hatuangukii kwenye mitego ambayo baadhi wanataka kutuvuta ndani yake,” alisema, akiongeza kuwa serikali inasimamia hali hiyo kwa tahadhari na utulivu huku ikiheshimu kanuni za ujirani mwema na mshikamano wa kikanda.
Rais huyo wa Uturuki alimkosoa vikali Waziri Mkuu wa Israel, Benjamin Netanyahu, akiishutumu uongozi wa Israel kwa kuchochea kutokuwa na utulivu na kudhoofisha amani ya kikanda.
“Mtandao wa mauaji unaoongozwa na Netanyahu lazima usitishwe mara moja kwa ajili ya amani ya kikanda na ubinadamu,” alisema Erdogan, akizitaka nchi duniani kuchukua msimamo wa kishujaa na wa kuchukua hatua mapema.
Alionya kuwa ingawa vita hivyo kimsingi ni vya Israel, athari zake zinahisiwa duniani kote.
“Siku 25 zilizopita zimeonyesha kuwa ingawa hii ni vita vya Israel, gharama yake inalipwa na dunia nzima,” alisema Erdogan. “Ni vita vya Netanyahu kwa ajili ya kuendelea kwake kisiasa, lakini mzigo huo unabebwa na watu bilioni nane.”
Erdogan pia alisisitiza umuhimu wa kimkakati wa Mlango wa Bahari wa Hormuz, njia muhimu ya kimataifa ya nishati ambapo takriban asilimia 20 ya biashara ya mafuta duniani hupita.
Alionya kuwa usumbufu katika usafirishaji kwenye mlango huo tayari umesababisha mtikisiko mkubwa katika uchumi wa dunia.
“Kufungwa kwa Mlango wa Bahari wa Hormuz, ambao ni muhimu kimkakati na ambapo asilimia 20 ya biashara ya nishati duniani hupita, kumesababisha mtikisiko mkubwa katika uchumi wa dunia,” alisema.
Erdogan alitoa wito wa kusitishwa mara moja kwa kile alichokiita vita visivyo halali kabla ya madhara yasiyoweza kurekebishwa kuathiri mfumo wa uchumi wa dunia.
“Vita lazima vikome kabla havijasababisha madhara makubwa kwa uchumi wa dunia ambayo yanaweza kuchukua miaka kurekebishwa,” alisema, akihimiza kufunguliwa haraka kwa njia za mazungumzo na kuanzishwa kwa mazungumzo yenye maana.
Pia alionya dhidi ya kuruhusu msimamo wa Israel kuzuia juhudi za kidiplomasia zinazolenga kutatua mgogoro huo.
“Msimamo usiobadilika, wa kiwango cha juu na mkali wa Israel haupaswi kuruhusiwa kuhujumu suluhisho za kidiplomasia,” alisema.
Licha ya kuongezeka kwa mvutano, Erdogan alisema Uturuki itaendelea kufanya kazi kwa ajili ya amani na utulivu kwa kutumia nyenzo zote za kidiplomasia na kisiasa zilizopo.
“Uturuki itaendelea kufanya kazi kwa nguvu zake zote na kwa njia zote ilizonazo kuleta amani, haki na utulivu,” alisema.
Rais huyo pia alizungumzia athari za kiuchumi za mgogoro huo, hasa kupanda kwa kasi kwa bei ya mafuta.
Alisema serikali inatekeleza hatua za kuwalinda raia wa Uturuki dhidi ya mshtuko wa uchumi wa dunia unaosababishwa na mzozo huo.
“Ili kuwalinda raia wetu dhidi ya mchakato huu unaoathiri dunia vibaya, tunatekeleza hatua kama mfumo wa kusawazisha bei ya mafuta,” alisema, akirejelea sera zinazolenga kupunguza athari za ndani za ongezeko la bei ya mafuta.
Erdogan aliongeza kuwa uchumi wa Uturuki kwa sasa una uimara wa kutosha kukabiliana na mishtuko ya nje.
“Mbele ya mishtuko isiyotabirika kama hii, kiwango cha uimara wa uchumi wa Uturuki sasa kiko katika kiwango cha juu zaidi katika historia yake,” alisema.
“Hakuna shaka kuhusu hilo.”














