Miaka kati ya 2015-2025 ndiyo miaka 11 yenye joto kali zaidi katika rekodi, na 2025 ulikuwa mwaka wa pili au wa tatu kwa joto zaidi katika rekodi, kwa takriban 1.43 °C.
Hii ni kwa mujibu wa Ripoti ya Hali ya Hewa Duniani 2025 iliyotolewa na Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO).
Ripoti ya Hali ya Hewa Duniani ya 2025 inategemea michango ya kisayansi kutoka kwa Huduma za Kitaifa za Hali ya Hewa, Vituo vya Hali ya Hewa vya Kanda vya WMO, washirika wa Umoja wa Mataifa na wataalamu kadhaa.
"Siku hadi siku, hali ya hewa yetu imekuwa mbaya zaidi. Mwaka 2025, joto, moto ya nyika, ukame, vimbunga vya kitropiki, dhoruba na mafuriko vilisababisha maelfu ya vifo, kuathiri mamilioni ya watu na kusababisha hasara ya mabilioni ya uchumi," Katibu Mkuu wa WMO Celeste Saulo alisema.
Kulingana na ripoti hiyo matukio makubwa duniani, ikiwa ni pamoja na joto kali, mvua kubwa na vimbunga vya kitropiki, yalisababisha usumbufu na uharibifu na kuangazia uwezekano wa kuathirika kwa uchumi na jamii.
Ripoti hiyo inaonesha kuwa bahari inaendelea kupata joto na kunyonya hewa ya kaboni dioksidi.
Imekuwa ikichukua sawa na takriban mara kumi na nane ya matumizi ya kila mwaka ya uwezo wa binadamu kila mwaka kwa miongo miwili iliyopita.
Ongezeko la joto zaidi duniani ni tishio
Kiwango cha barafu cha bahari kwa mwaka katika Arctic kilikuwa chini au karibu na rekodi ya chini, kiwango cha barafu ya bahari ya Antarctic kilikuwa cha tatu kwa rekodi, na kuyeyuka kwa barafu kuliendelea, kulingana na ripoti hiyo.
"Hali ya Hewa Duniani iko hatarini. Sayari ya Dunia inasukumwa kupita mipaka yake. Kuna kila kiashirio cha hatari katika hali ya hewa," Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres alisema.
WMO inasema ongezeko la joto la anga hewa ikiwa ni pamoja na karibu na uso wa Dunia (joto ambalo wanadamu wanahisi) linawakilisha 1% tu ya nishati ya ziada, wakati karibu 5% imehifadhiwa katika ardhi ya bara.
Zaidi ya 91% ya joto la ziada huhifadhiwa katika bahari, ambayo huwa ni kama kinga kuu dhidi ya joto la juu zaidi ardhini.
Ripoti za WMO zinaonesha kuwa kiwango cha joto baharini kilifikia rekodi mpya ya juu mwaka 2025 na kiwango cha ongezeko la joto kiliongezeka zaidi ya mara mbili kutoka 1960-2005 hadi 2005-2025.
"Binadamu ndio wamestahimili miaka kumi na moja ya joto zaidi katika rekodi. Historia inapojirudia mara kumi na moja, si bahati mbaya tena. Ni wito wa kuchukua hatua," alisema Guterres.
Viwango vya barafu kwenye Antaktika na Greenland zote zimepoteza uzito mkubwa na kiwango cha wastani cha barafu cha bahari ya Arctic kwa mwaka wa 2025 kilikuwa cha chini zaidi au cha pili zaidi.
Upotevu wa kipekee wa barafu ulitokea Iceland na pwani ya Pasifiki ya Amerika Kaskazini mnamo 2025.
"Na katika enzi hii ya vita, changamoto ya hali ya hewa pia inafichua ukweli mwingine: uraibu wetu wa nishati ya mafuta unavuruga hali ya hewa na usalama wa kimataifa. Ripoti ya leo inapaswa kuja na tahadhari: machafuko ya hali ya hewa yanaongezeka na kuleta hatari," alisema Guterres.
Bahari inayoongezeka joto na barafu inayoyeyuka inaripotiwa kusababisha kupanda kwa wastani wa kina cha bahari duniani, ambacho kimeongezeka tangu vipimo vya satelaiti kuanza mwaka 1993.
Ongezeko la joto la bahari na kupanda kwa kina cha bahari kutaendelea kwa karne nyingi, kulingana na makadirio ya Jopo la Serikali za Kimataifa kuhusu Mabadiliko ya Tabianchi (IPCC).









