Kikosi cha jeshi kilichokuwa kikiasi kilitangaza Jumapili kwamba kinachukua udhibiti wa vikosi vyote vya kijeshi vya Madagascar huku Rais Andry Rajoelina akisema kuwa "jaribio la kuchukua madaraka kinyume cha sheria" linaendelea.
Kikosi cha CAPSAT, ambacho kinajumuisha maafisa wa kiutawala na kiufundi, kilijiunga na maelfu ya waandamanaji katikati mwa jiji Jumamosi, hatua kubwa katika harakati za zaidi ya wiki mbili za kupinga serikali.
Awali, kikosi hicho kilitangaza kwamba "kitakataa amri za kufyatua risasi" na kilikosoa gendarmerie, ambao wameshutumiwa kwa kutumia mbinu za nguvu kupita kiasi dhidi ya waandamanaji, hali iliyosababisha vifo kadhaa.
Lakini Jumapili, maafisa wa CAPSAT walidai katika taarifa ya video kwamba "kuanzia sasa, maagizo yote ya jeshi la Madagascar – iwe ardhini, angani au baharini – yatatoka makao makuu ya CAPSAT."
Maafisa hao walisema wamemteua Jenerali Demosthene Pikulas kama mkuu wa jeshi – nafasi ambayo ilikuwa wazi tangu mkuu wa zamani alipoteuliwa kuwa waziri wa vikosi vya ulinzi wiki iliyopita – ingawa haikufahamika wazi ikiwa uteuzi huo unaweza kuchukuliwa kuwa rasmi.
Wanajeshi waungana na waandamanaji mitaani
Hakukuwa na majibu ya haraka kutoka kwa vitengo vingine au uongozi wa sasa wa kijeshi.
Wanajeshi kutoka kikosi hicho walipambana na gendarmerie nje ya kambi Jumamosi na wakaingia jijini kwa magari ya jeshi kujiunga na waandamanaji, ambao waliwapokea kwa shangwe na wito wa kumtaka Rajoelina ajiuzulu.
Mkusanyiko mwingine na ibada ya maombi vilifanyika tena katika mji mkuu Jumapili.
Rais alitoa taarifa Jumapili akisema "jaribio la kuchukua madaraka kinyume cha sheria na kwa nguvu, kinyume na katiba na kanuni za kidemokrasia, linaendelea."
'Makosa'
"Mazungumzo ndiyo njia pekee ya kusonga mbele na suluhisho pekee kwa mgogoro unaoikabili nchi kwa sasa," alisema, akitoa wito wa "umoja."
Mapema Jumapili, maafisa wa gendarmerie walisema katika taarifa ya video kwamba wanatambua "makosa na kupita kiasi katika hatua zetu," wakitoa wito wa "undugu" kati ya jeshi na gendarmerie.
"Tuko hapa kulinda, si kutisha," walisema, wakiongeza kuwa "kuanzia sasa, maagizo yote yatatoka pekee" kutoka makao makuu ya gendarmerie.
Maandamano ya Jumamosi katika mji mkuu Antananarivo yalikuwa moja ya makubwa zaidi tangu harakati za maandamano zilipoanza Septemba 25, zikichochewa na hasira juu ya ukosefu wa umeme na maji.
Serikali yasema iko 'tayari kushirikiana na kusikiliza'
Jumamosi usiku, serikali ilihakikisha kwamba Rajoelina bado "yuko nchini" na anasimamia masuala ya kitaifa, huku waziri mkuu mpya akisema serikali "inasimama imara" na "iko tayari kushirikiana na kusikiliza."
Kikosi cha CAPSAT kiko katika wilaya ya Soanierana pembezoni mwa Antananarivo.
Kambi hiyo hiyo ya kijeshi mwaka 2009 iliongoza uasi wakati wa maandamano ya umma yaliyomleta Rajoelina madarakani.
Tume ya Umoja wa Afrika Jumapili ilionyesha "wasiwasi mkubwa" juu ya hali ya Madagascar.
AU yatoa wito wa 'utulivu na uvumilivu'
"Mwenyekiti wa Tume anakaribisha ahadi mpya ya Serikali kwa mazungumzo na anatoa wito kwa wadau wote wa Malagasy, wa kiraia na kijeshi, kudumisha utulivu na uvumilivu," ilisema katika taarifa.
Jirani Afrika Kusini pia ilitoa wito kwa "pande zote kuheshimu mchakato wa kidemokrasia na utaratibu wa kikatiba."
Umoja wa Mataifa umesema kwamba angalau watu 22 waliuawa katika siku za kwanza za maandamano yaliyoanza Septemba 25.
Rajoelina amepinga idadi hiyo, akisema wiki iliyopita kulikuwa na "vifo 12 vilivyothibitishwa na wote walikuwa waporaji na waharibifu."
Kulingana na vyombo vya habari vya ndani, huduma za dharura ziliripoti vifo vingine viwili na majeruhi 26 Jumamosi. Kikosi cha CAPSAT kilisema mwanajeshi mmoja pia alipigwa risasi na gendarmerie na kufariki.